Mchango wa nyimbo za muziki wa dansi za muhiddin maalim gurumo katika malezi ya vijana nchini Tanzania
Date
Authors
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
Abstract
Lengo kuu la utafiti wetu lilikuwa kuchunguza mchango wa nyimbo za Muhidin Gurumo katika malezi ya vijana nchini Tanzania. Sanjari na lengo hilo kuu, pia tuliweka malengo mahsusi matatu. Lengo la kwanza ni kubainisha nyimbo za Muhiddin Gurumo zinazohusu malezi ya vijana. Pili ni kuchambua mchango wa nyimbo za Muhiddin Gurumo katika malezi ya vijana. Na lengo la tatu ni kuchunguza mustakabali wa nyimbo hizo katika malezi ya vijana. Utafiti wetu tulianzia maktabani na baadaye tulienda kukusanya data uwandani katika jiji la Dar es Salaam. Vifaa vilivyotumika katika ukusanyaji wa data ni kama vile shajara, kamera ya picha tuli na sogezi, kalamu na karatasi na kompyuta. Data za utafiti huu zilipatikana kwa kufanya usaili na majadiliano na watafitiwa, kusikiliza redio, na diga za nyimbo za dansi na ushuhudiaji jukwaani. Data za utafiti huu zilichambuliwa kwa kutumia nadharia za usosholojia na uhalisia na mkabala wa kimaelezo. Baada ya hatua hizo, tulibaini kuwa nyimbo za muziki wa dansi za Muhiddin Maalim Gurumo ni nyingi na zina mchango mkubwa katika malezi ya vijana. Baadhi ya mchango wa nyimbo hizo ni kuwaasa vijana waache anasa, wathamini wazazi, waache uzururaji, wawe wavumilivu, wawajibike na wathamini elimu. Mwishoni, utafiti wetu umetoa ushauri kwa jamii, watafitiwa, wasanii na wadau wa muziki wa dansi kuendelea kutunga nyimbo za kuwaasa na kuwaonya vijana ili jamii ipate mafanikio zaidi.