Matatizo ya kiutendaji yanayoikabili taaluma ya ukalimani wa mikutano

Date

2013

Journal Title

Journal ISSN

Volume Title

Publisher

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam

Abstract

Lengo kuu la utafiti huu lilihusu kuchunguza Matatizo ya Kiutendaji katika Ukalimani wa Mikutano yanayoikabili Taaluma ya Ukalimani. Maswali matatu yalitumika: (i) Kuchunguza matatizo ya kiutendaji katika ukalimani wa mikutano, (ii) Kubainisha athari zinazotokana na matatizo ya kiutendaji katika ukalimani wa mikutano na (iii) Kupendekeza mbinu za kupunguza matatizo ya kiutendaji katika ukalimani wa mikutano ili kuiboresha taaluma hii. Utafiti huu ulihusisha zaidi mkabala usio wa kiidadi lakini kuna mchanganyiko pia wa mkabala wa kiidadi. Jumla ya walengwa 41 wakiwemo wakalimani 9 wa Bunge la Afrika na Umoja wa Afrika, wakalimani 5 wa hapa nchini Tanzania, wakalimani 2 wa mikutano nje ya nchi, mwandaaji mikutano 1, na fundi wa mitambo ya ukalimani 1, na washiriki wa mikutano 23 katika maeneo ya Umoja wa Afrika na Bunge la Afrika walitumiwa kujibu maswali. Walengwa walichaguliwa kimakusudi ili kupata data zenye kulenga tatizo la utafiti. Data zilikusanywa kwa njia ya mahojiano, madodoso na uchunguzi uliofaywa na mtafiti uwandani. Uchambuzi wa kiidadi na usio wa kiidadi ulifanyika. Matokeo ya utafiti yalionyesha kwamba kuongea kwa haraka, mazingira ya kiufundi na kiutendaji yalisababisha vikwazo vilivyochangia katika kupotosha maana na kuharibu mawasiliano baina ya wakalimani na washiriki. Imebainika kuwa tatizo sugu lilikuwa ni kushindwa kuwasilisha maana iliyokusudiwa kulikosababishwa na kuongea kwa haraka, lafudhi kuwa mbaya, kutokuelewa ujumbe vizuri, vikwazo katika mazingira ya kazi ya ukalimani kama vile kutokutoa nakala za nyaraka mapema kabla ya mkutano, kucheleweshwa kwa malipo na posho za wakalimani, muda wa kazi kuwa mrefu na yale yanayohusu ufundi na maandalizi, mafunzo kwa wakalimani kukosekana, kukosa chama cha wakalimani na, kukosekana ujuzi wa kutumia vifaa vya ukalimani vizuri. Hivyo lugha zilizosikilizwa sana na washiriki ni Kiswahili (87 %), Kiingereza (82.6%) na Kifaransa (26.1%). Ilielezwa wazi pia kuwa kutokumudu lugha vizuri kuliharibu mawasiliano mazuri baina ya washiriki na wakalimani. Athari kuu ni upotoshaji wa maana na vikwazo katika kazi ambapo mbinu tegemezi zimebainishwa kuwa ni (i) kuondoa vikwazo katika kazi, (ii) mkakati wa kuepusha upotoshaji wa maana kwa kuzingatia vigezo na masharti vinavyotakiwa katika kazi hii, (iii) kuboresha dhana za kazi, (iv) mafunzo kwa wakalimani kuandaliwa katika ngazi husika za elimu, na (v) kuthamini lugha ya Kiswahili. Utafiti ulipendekeza kwamba ufumbuzi wa matatizo ya wakalimani usihusu wakalimani peke yao bali ushirikishe wadau wote wakiwemo walengwa katika utafiti huu: wakalimani na washiriki, serikali na taasisi zinazohusika na masuala ya lugha ndani na nje ya nchi katika bara la Afrika, kwa kuwa vyanzo vya matatizo ni vingi na vimeshamiri. Aidha pendekezo limetolewa la kufanya utafiti mwingine zaidi wa kujuwa ufanisi wa wakalimani wa lugha ya Kiswahili kwenye mikutano ya Afrika.

Description

Keywords

Swahili language, Transilating services

Citation

Mwaituka, D. P (2013) Matatizo ya kiutendaji yanayoikabili taaluma ya ukalimani wa mikutano, Tasinifu ya M.A Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Kinapatikana http://41.86.178.3/internetserver3.1.2/detail.aspx)