Ufaafu wa mifano ya matumizi kwenye kamusi ya kiswahili sanifu (TUKI, 2013) katika kupata maana ya kidahizo mifano kutoka shule za sekondari
Date
Authors
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
Abstract
Kamusi inasaidia kuifahamu lugha vizuri kwa kuvitumia vipengele mbalimbali vya kiisimu. Vipengele vinavyoangaliwa kwenye kamusi ni pamoja na maana ya neno, kategoria, matamshi, ngeli za nomino na mifano ya matumizi. Utafiti huu unahusu Ufaafu wa Mifano ya Matumizi kwenye Kamusi ya Kiswahili Sanifu (TUKI, 2013) katika Kupata Maana ya Kidahizo: Mifano Kutoka Shule za Sekondari. Data za utafiti huu zimekusanywa kwa njia ya hojaji na mahojiano katika shule nane za sekondari wilayani Nyamagana mkoani Mwanza. Aidha, utafiti ulikuwa na malengo yafuatayo: kubainisha uwezo wa wanafunzi wa kutambua mifano ya matumizi iliyomo kwenye KKS (TUKI, 2013), kueleza ni kwa kiasi gani wanafunzi wanaelewa umuhimu wa mifano ya matumizi iliyomo kwenye KKS (TUKI, 2013) na kujadili ufaafu wa mifano ya matumizi katika KKS (TUKI, 2013) kwa wanafunzi na walimu katika shule za sekondari. Utafiti huu umeongozwa na Nadharia ya Maana kama Matumizi. Matokeo ya utafiti yanaonesha kwamba wanafunzi wa shule za sekondari wanaweza kuitambua mifano ya matumizi kwenye kamusi kwa kuangalia namna inavyoandikwa, kusoma utangulizi wa kamusi, kuangalia sentensi zilizo na rangi na kuangalia alama ya wimbi. Vilevile, imebainika kuwa wanafunzi wana uelewa kuhusu mifano ya matumizi kwa kuwa waliweza kueleza umuhimu wa mifano hiyo inavyowasaidia kupata maana ya kidahizo. Pia, data za utafiti huu zimedhihirisha kwamba mifano ya matumizi ni faafu kwa wanafunzi na walimu. Inawasaidia kujifunza maana ya kidahizo, miundo ya sentensi, kuongeza uwezo wa kufikiri, kujifunza semi na kurekebisha makosa mbalimbali ya matumizi ya lugha. Hali kadhalika, walimu huitumia mifano hiyo kufundisha lugha ya Kiswahili kwenye vipengele vya utungaji wa sentensi, maana ya kidahizo na kuondoa utata wa maneno. Kutokana na data za utafiti huu inapendekezwa kuwa matumizi ya kamusi katika shule za sekondari yaboreshwe kwani ni nyenzo muhimu ya kujifunzia lugha.