Matumizi na dhima za lugha zilizoandikwa kwenye bodaboda: mifano kutoka jiji la Dar es Salaam.
Date
Authors
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
Abstract
Utafiti huu unahusu matumizi na dhima za lugha zilizoandikwa kwenye bodaboda, mifano kutoka Jiji la Dar es Salaam na ulifanyika katika kata tatu wilayani Kinondoni, yaani Ubungo, Kimara Mwisho na Mbezi Mwisho. Utafiti huu ulijikita katika malengo mahususi mawili. Mosi, kubainisha lugha zilizoandikwa kwenye bodaboda na pili kueleza dhima za lugha hizo. Ili kufanikisha kazi hii, Nadharia ya Uchunguzi Tunduizi ya Kilongo ilitumika kubaini dhima za lugha kwa kuhusishwa na muktadha wa kijamii. Utafiti huu umegawanyika katika sura tano. Sura ya kwanza imeeleza kiini cha utafiti na utaratibu uliozingatiwa katika kufanikisha utafiti. Sura ya pili imeshughulikia mapitio ya maandiko kuhusiana na maandishi ya sehemu za umma. Sura ya tatu imehusu mbinu za utafiti ambapo populesheni, sampuli, usampulishaji pamoja na njia tatu za ukusanyaji wa data zilibainishwa. Sura ya nne imeshughulikia uchanganuzi na uwasilishaji wa data. Kwa ujumla data iliyopatikana imechanganuliwa kwa mkabala wa kimaelezo pamoja na majedwali na vielelezo. Sura ya tano imeshughulikia muhtasari, hitimisho na mapendekezo. Matokeo ya utafiti huu yamedhihirisha kuwa lugha zilizoandikwa kwenye bodaboda katika eneo la utafiti zimesheheni matumizi ya wingilugha. Lugha hizo ni Kiswahili, Kiingereza, Kiarabu, Lugha za Makabila, Kilingala na mchanganyiko wa lugha nyingine, mfano Kilingala na Kiswahili. Vilevile, dhima zilizowasilishwa kwa kutumia lugha hizo ni pamoja na imani na shukurani kwa Mungu, uvumilivu na ujasiri, maadili, utambulisho, mapenzi na ndoa, bidii katika kazi na umuhimu wa kufanya mazoezi. Mwisho, utafiti huu umetoa mapendekezo yafuatayo: kuchunguza mantiki na matumizi ya michoro isiyo na maandishi, lugha ya picha pamoja na makosa ya kisarufi kwenye sehemu za umma. Utafiti huu pia umefanywa Jijini Dar es Salaam, hivyo tafiti nyingine zinaweza kufanywa katika mikoa mingine nchini Tanzania na nje ya Tanzania.