Ulinganishi wa kiisimu wa lugha ya Samatengo na ya Kindendeule
No Thumbnail Available
Date
2013
Authors
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
University of Dar es Salaam
Abstract
Madai kwamba lugha ya Samatengo na ya Kindendeule zinafanana yamekuwapo kwa
muda mrefu miongoni mwa wanaisimu, wachunguzi na wazungumzaji wa Samatengo
na Kindendeule. Utafiti huu ulihusu Ulinganishi wa Kiisimu wa Lugha ya Samatengo
na ya Kindendeule. Tatizo la utafiti lilikuwa ni kutafuta data za kiisimu kutoka
uwandani ili kuhakiki madai kwamba lugha ya Samatengo na ya Kindendeule
zinafanana. Lengo kuu lilikuwa kuonesha ni kwa kiwango gani Samatengo na
Kindendeule zinafanana kiisimu ili kufahamu hadhi ya kila moja katika muktadha wa
uhususiano wake. Kulikuwa na malengo mahususi matatu. Moja, kuweka vigezo vya
kubainisha msingi wa kufanana kwa Samatengo na Kindendeule. Pili, kueleza
mwelekeo unaotokana na kufanana kwa vigezo vilivyowekwa. Tatu, kuthibitisha kama
hizi ni lugha mbili tofauti au ni lahaja za lugha moja. Data kwa ajili ya utafiti huu
zilikusanywa kwa kutumia njia tatu ambazo ni maandishi maktabani, hojaji na
majadiliano ya vikundilengwa. Mbinu za uchambuzi wa data zilizotumika ni mbinu ya
takwimuleksika, mbinu linganishi, na mbinu ya maelezo, ambazo zilikuwa
zikikamilishana. Matokeo kwa jumla yamesaidia kujibu maswali ya utafiti na kufikia
malengo yaliyowekwa. Lengo la kwanza na swali la kwanza lilihusu vigezo vya
kubainisha kufanana kwa Samatengo na Kindendeule. Vigezo viwili vilitumika
ambavyo ni msamiati wa msingi na ukubaliano wa sauti. Lengo la pili na swali la pili
lilihusu mwelekeo unaotokana na kiwango cha kufanana kwa vigezo vilivyowekwa;
imewekwa wazi kwamba mwelekeo ni wa uhusiano wa karibu zaidi kiasi cha
kuhitimisha kuwa ni lahaja za lugha moja ya azali. Lengo la tatu na swali la tatu lilihusu
kuthibitisha kama hizo ni lugha mbili au ni lahaja za lugha moja. Imethibitishwa kwa
vigezo vya kiisimu kuwa Samatengo na Kindendeule ni lahaja za lugha moja. Utafiti
unaonesha kwamba Samatengo na Kindendeule zinafanana kwenye kigezo cha
msamiati wa msingi kwa 87%. Pia zinafanana katika kigezo cha fonimu za konsonanti
kwa asilimia 75% na katika kigezo cha fonimu za irabu kwa 100%. Fasili ya viwango
hivyo vya asilimia za kufanana ni kwamba Samatengo na Kindendeule ni lahaja za
lugha moja ya azali. Inapendekezwa kwanza, kwa kuwa utafiti huu ulihusu ulinganishi
wa Samatengo na Kindendeule, ufanyike utafiti mwingine katika kulinganisha lugha
nyingine zinazodaiwa kufanana ili kuweka wazi kiwango cha uhusiano kilichopo baina
ya lugha hizo kwa ajili ya kupanua maarifa ya isimu. Pili, inapendekezwa ufanyike
utafiti mwingine utakaosaidia kubaini lugha azali kwayo Samatengo na Kindendeule
zilitokana nayo. Tatu, utafiti huu ulilinganisha vipengele viwili vya kiisimu yaani
msamiati wa msingi na ukubaliano wa sauti. Hivyo ufanyike utafiti mwingine kwa
kutumia vigezo vya sintaksia, mofololojia na semantiki ili kubaini kiwango cha
kufanana baina ya Samatengo na Kindendeule katika vipengele hivyo. Nne, ufanyike
pia utafiti mwingine ili kubaini athari za kihistoria na kiisimujamii katika lahaja za
Samatengo na Kindendeule.
Description
Available in print form
Keywords
Bantu languages, Matengo language, Ndendeuli language, Languages, Tanzania
Citation
Kawonga, G (2013) Ulinganishi wa kiisimu wa lugha ya Samatengo na ya Kindendeule, Tasinifu ya M.A (Kiswahili), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. (Kinapatikana http://41.86.178.3/internetserver3.1.2/detail.aspx)