Kirai kitenzi cha kibantu ulinganishi wa muundo wa kirai kitenzi cha Kiswahili na Kizigua

No Thumbnail Available
Date
2014
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
University of Dar es Salaam
Abstract
Utafiti huu ulilenga kulinganisha muundo wa Kirai Kitenzi cha Kiswahili na Kirai Kitenzi cha Kizigua. Utafiti ulichunguza kufanana na kutofautiana kwa muundo wa virai vitenzi hivyo na vipashio mbalimbali vinavyoandamana nacho. Katika utafiti huu tumetumia hojaji, majadiliano, ushuhudiaji na ushiriki wa mazungumzo ya wazigua wazawa ili kupata data ambapo watoa taarifa 40 kutoka vijiji vya Misima, Kwachaga, Suwa, Chogo, Chogo-Makazi, Mdoe na Vibaoni walishirikishwa. Nadharia iliyotuongoza katika uchanganuzi wa data ni nadharia ya Sarufi Miundo Virai Jumuishi (SMVJ) iliyoanzishwa mwaka 1970 na Gerald Gazdar, inayotumika kuelezea sintaksia ya lugha. Nadharia hii inaachana na sarufi zilizozingatia ugeuzaji maumbo na sheria za muundo virai na badala yake inatumia kanuni ya utawala wa moja kwa moja na kanuni ya utangulizani katika kuchunguza muundo wa kirai kitenzi cha Kizigua ili kuonesha uhusiano wa kiwima na kiulalo uliopo baina ya kitenzi na vipashio vinavyoandamana nacho. Matokeo yamebaini miundo 17 ya kirai kitenzi cha Kizigua, ambapo ipo miundo ambayo kitenzi huweza kusimama peke yake bila kufuatiwa na kipashio chochote. Ipo pia miundo ambayo kitenzi chake kinaweza kufuatiwa na vipashio mbalimbali. Matokeo pia yanaonesha kuwa vipo vipashio vya aina mbalimbali vinavyoweza kuandamana na kitenzi cha Kizigua. Vipashio hivyo ni pamoja na kikundi nomino, kikundi kielezi, kikundi kihusishi, kitenzi kisaidizi, kishazi tegemezi na hata sentensi. Pia, matokeo yanaonesha kuwa kuna kufanana na kutofautiana baina ya miundo ya kirai kitenzi cha Kizigua na ile ya kirai kitenzi cha Kiswahili, ambapo miundo 14 kati 17 ya Kirai Kitenzi cha Kizigua ambayo ni sawa na 82.4% inafanana na miundo ya kirai kitenzi cha Kiswahili na miundo mitatu kati ya 17 ya KTZ ambayo ni 17.6% inatofautiana na ile ya Kiswahili. Tumebaini pia kuwa karibu kila kitenzi cha Kizigua kinaweza kuwa na dhima ya uelekezi, yaani kinaweza kuwa kitenzi elekezi au si elekezi. Hii ina maana kwamba si lazima kwa kitenzi cha Kizigua na hata cha Kiswahili kiwe na uyambwa, yaani kuwa na uwezo wa kuchukua nomino, bali kinaweza kuchukua vipashio vingine visivyokuwa yambwa kama vile kikundi kielezi na kikundi kihusishi.
Description
Available in print form, East Africana Collection, Dr. Wilbert Chagula Library, Class mark (THS EAF PL8025.A22)
Keywords
Swahili literature, Zigua language, Bantu language
Citation
Abdallah, N. (2014) Kirai kitenzi cha kibantu ulinganishi wa muundo wa kirai kitenzi cha Kiswahili na Kizigua, Master dissertation, University of Dar es Salaam. Dar es Salaam.