Mandhari na usawiri wa ukimwi katika riwaya ya kiswahili 2000-2010

Loading...
Thumbnail Image
Date
2016
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
University of Dar es Salaam
Abstract
Utafiti huu umechunguza jinsi ugonjwa wa UKIMWI unavyosawiriwa katika fasihi kwa kuiangalia riwaya ya Kiswahili kupitia katika kipengele cha mandhari. Utafiti unalenga kujibu maswali yafuatayo: kwanza, ni jinsi gani mandhari ya riwaya ya Kiswahili ihusuyo UKIMWI inafungamana na dhamira zinazosawiriwa na riwaya husika? Pili, riwaya ya Kiswahili ihusuyo UKIMWI inatumiaje mandhari kuumba wahusika wake? Na mwisho, waandishi wa riwaya ya Kiswahili ihusuyo UKIMWI wanatumiaje mandhari kujenga lugha inayoibua athari na changamoto za UKIMWI katika riwaya zao? Sambamba na maswali hayo, tumefafanua malengo ya utafiti huu kuwa ni: mosi, kujadili jinsi mandhari inavyofungamana na dhamira zinazoelezwa na riwaya ya Kiswahili ihusuyo UKIMWI. Pili, kueleza jinsi riwaya ya Kiswahili ihusuyo UKIMWI inavyotumia mandhari kuumba wahusika wake. Na tatu ni kubainisha namna waandishi wa riwaya ya Kiswahili ihusuyo UKIMWI wanavyotumia mandhari kuumba lugha inayoibua athari na changamoto za UKIMWI katika riwaya zao. Ili kufikia kusudi la utafiti huu , tumetumia mbinu mbalimbali za utafiti zikiwamo za utafiti wa nyaraka na mahojiano. Mbinu hizi kwa pamoja zimetumika kukusanya data zilizosaidia kujibu maswali ya utafiti huu. Nadharia ya Mwingiliano-matini ndiyo imeongoza utafiti huu. Nadharia hii inasisitiza kuwa hakuna matini asilia, bali uhai wa matini moja hutegemea matini nyingine. Kwa hiyo, matini za kifasihi hutegemeana katika kukamilisha maana. Kwa kutumia nadharia hii tumeona kuwa, mandhari zinaingiliana, kukamilishana na kutegemeana katika kuliumba tatizo la UKIMWI. Hii inatokana na ukweli kuwa, riwaya zinazochunguzwa zimetumia mandhari mbalimbali kuwaumba wahusika, kuibua dhamira na kuchomoza lugha inayoelezea athari na changamoto za UKIMWI. Kutokana na utafiti huu, upo uhusiano mkubwa kati ya mandhari na uibuaji wa dhamira za kazi ya fasihi. Pili, kuna uhusiano kati ya mandhari na ujenzi wa wahusika. Wasifu, tabia na mienendo ya wahusika wa riwaya teule kwa sehemu kubwa ni matokeo ya mandhari wanamokuwa. Vilevile, mandhari inahusiana na lugha kwani, lugha inayotumiwa na wahusika katika riwaya inategemea mandhari wanamokuwa. Hii inathibitisha kuwa, mandhari ina umuhimu mkubwa katika kuibua dhamira, kuwaumba wahusika pamoja na kutolea ujumbe uliokusudiwa katika kazi ya fasihi hasa riwaya. Kutokana na uchunguzi wa riwaya teule, kazi ya fasihi hasa riwaya haikamilishwi na mandhari moja, bali upo mwingiliano mkubwa wa mandhari mbalimbali ambao unaifanya riwaya ikamilishe maana na kusudi la mwandishi. Na kwa hiyo, mandhari ni mojawapo ya mihimili muhimu katika kuumba maana ya kazi ya fasihi.
Description
Available in print form, East Africana Collection, Dr. Wilbert Chagula Library, Class mark (THS EAF PL8703.5.B84)
Keywords
Swahili literature, Aids (Disease)
Citation
Bulaya, J. (2016) Mandhari na usawiri wa ukimwi katika riwaya ya kiswahili 2000-2010, Tasnifu ya uzamivu, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dar es Salaam
Collections