Michakato ya kisemantiki kwenye maneno ya mkopo katika kiswahili: mifano kutoka Kiingereza na Kiarabu

Loading...
Thumbnail Image
Date
2017
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
University of Dar es Salaam
Abstract
Kiswahili kama zilivyo lugha nyingine kimekopa maneno kutoka lugha mbalimbali. Miongoni mwa lugha hizo ni Kiingereza na Kiarabu. Maneno hayo yanapoingia katika Kiswahili huchakatwa katika viwango mbalimbali vya kiisimu kama vile kifonolojia, kimofolojia na kisemantiki ili yaendane na mfumo wa lugha ya Kiswahili. Utafiti huu umechunguza michakato ya kisemantiki inayojitokeza kwenye maneno ya mkopo katika Kiswahili ili kubainisha njia za kutambua maneno ya mkopo katika Kiswahili, kanuni za kuwakilisha michakato hiyo, sababu za kutokea kwa michakato hiyo na kuonesha tofauti za utokeaji wa michakato ya kisemantiki kati ya maneno yenye asili ya Kiingereza na yale yenye asili ya Kiarabu. Utafiti huu uliongozwa na nadharia mbili ambazo ni Nadharia ya Alama na Nadharia ya Sarufi Amilifu. Kwa kiasi kikubwa data zilikusanywa kwa kutumia mbinu ya maktabani ambapo data zilizopatikana kwa mbinu hiyo ndio zilipelekwa uwandani kuhakikiwa kwa kutumia mbinu za hojaji na usaili. Uchambuzi wa data ulitumia mbinu ya uchambuzi mada ambapo maelezo ndio yametumika kwa kiasi kikubwa japo kulikuwa na matumizi ya kanuni, majedwali na vielelezo. Matokeo ya utafiti huu yanadhihirisha kuwa maneno ya mkopo yaliyomo katika Kiswahili yanaweza kubainishwa kwa kutumia njia za kileksikografia, kifonolojia na kimatamshi. Vilevile, utafiti huu umebaini kuwa tunaweza kuibainisha michakato mikuu minne ya kisemantiki kwa kutumia kanuni mbalimbali. Mathalani, kuna kanuni ya kubainishia Mchakato Panuzi wa Kisemantiki (MPK), Mchakato Finyazi wa Kisemantiki (MFK), Mchakato Geuzi wa Kisemantiki (MGK) na Mchakato Kapa wa Kisemantiki (MKK). MFK umeonekana kuchakata idadi kubwa ya maneno ya mkopo kuliko mingine. MFK umechakata 84% ya maneno yenye asili ya Kiingereza na 64% ya maneno yenye asili ya Kiarabu. Mchakato unaofuatia ni MPK umechakata 8% ya maneno yenye asili ya Kiingereza na 20% yenye asili ya Kiarabu. MGK umechakata 0% ya maneno yenye asili ya Kiingereza na 14% yenye asili ya Kiarabu ilhali MKK umechakata 8% ya maneno yenye asili ya Kiingereza na 2% yenye asili ya Kiarabu. Pia, matokeo yameonesha kuwa kuna sababu mahususi za kutokea kwa michakato ya kisemantiki kwenye maneno ya mkopo na utokeaji wa michakato hiyo katika maneno ya mkopo unatofautiana kati ya lugha kopwaji moja na nyingine. Aidha, utafiti huu unapendekeza kuwa tafiti fuatishi ziangalie michakato ya kisemantiki katika maneno yenye asili ya Kibantu katika Kiswahili, kwani utafiti huu umechunguza yale tu yenye asili ya Kingereza na Kiarabu.
Description
Available in print form, East Africana Collection, Dr. Wilbert Chagula Library, Class mark (THS EAF PL8702.S453)
Keywords
Swahili language, Grammar, Semantics, English language, Arabic language
Citation
Shembilu, M. M. (2017) Michakato ya kisemantiki kwenye maneno ya mkopo katika kiswahili: mifano kutoka Kiingereza na Kiarabu, Tasnifu ya uzamivu, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dar es Salaam
Collections