PhD Theses
Permanent URI for this collection
Browse
Browsing PhD Theses by Subject "English language"
Now showing 1 - 2 of 2
Results Per Page
Sort Options
Item Athari za kiutamaduni katika tafsiri mifano kutoka matini za Kitalii katika makumbusho za Tanzania(University of Dar es Salaam, 2014) Jilala, HadijaUtafiti huu umeshughulikia athari za kiutamaduni zijibainishazo katika tafsiri kwa kuchambua matini za kitalii zilizopo katika Makumbusho za Tanzania. Nia ya kufanya hivyo ni kuibua modeli ya kutafsiri matini za kiutamaduni ambayo itakuwa kiunzi cha kutafsiri matini za kiutamaduni ili kudhibiti mapungufu ya kimawasiliano. Dira iliyoongoza katika utengenezaji wa modeli ni matokeo ya utafiti huu na mhimili wa mawazo ya Nadharia ya Skopos. Ili kuibua Modeli ya Mawasiliano ya Kiutamaduni, tulitathmini mbinu za kutafsiri matini za kiutamaduni, mikakati iliyotumika katika uteuzi wa visawe vya kiutamaduni, mapungufu ya kimawasiliano yanayosababishwa na athari za kiutamaduni na namna tunavyoweza kukabiliana nayo. Data za utafiti huu zilipatikana kwa kutumia mbinu za usomaji wa machapisho, dodoso, usaili, uchunguzi shirikishi na upimaji. Utafiti huu umegundua kuwa, mbinu zinazotumika kutafsiri matini za kiutamaduni hazina uangavu na hivyo kusababisha mapungufu mengi ya kimawasiliano. Kichochezi kikuu cha mapungufu ya kimawasiliano ni mwachano wa kiutamaduni baina ya utamaduni chanzi na utamaduni lengwa. Ili kupunguza dosari hizo, utafiti huu umependekeza Modeli ya Mawasiliano ya Kiutamaduni (MMK) ambayo ni kiunzi cha kutafsiri matini za kiutamaduni ili kuleta ufanisi wa mawasiliano. Mhimili mkuu wa modeli hii ni fikra kwamba, ujumbe wa matini ya kiutamaduni ndiyo huukilia mbinu za tafsiri. Aidha, utafiti huu umebaini kuwa mbinu inayofaa kutafsiri matini za kiutamaduni ni “uasilishaji na ufafanuzi wa visawe”. Mbinu hii ndiyo nguzo kuu ya Modeli ya Mawasiliano ya Kiutamaduni.Item Michakato ya kisemantiki kwenye maneno ya mkopo katika kiswahili: mifano kutoka Kiingereza na Kiarabu(University of Dar es Salaam, 2017) Shembilu, Musa MohamedKiswahili kama zilivyo lugha nyingine kimekopa maneno kutoka lugha mbalimbali. Miongoni mwa lugha hizo ni Kiingereza na Kiarabu. Maneno hayo yanapoingia katika Kiswahili huchakatwa katika viwango mbalimbali vya kiisimu kama vile kifonolojia, kimofolojia na kisemantiki ili yaendane na mfumo wa lugha ya Kiswahili. Utafiti huu umechunguza michakato ya kisemantiki inayojitokeza kwenye maneno ya mkopo katika Kiswahili ili kubainisha njia za kutambua maneno ya mkopo katika Kiswahili, kanuni za kuwakilisha michakato hiyo, sababu za kutokea kwa michakato hiyo na kuonesha tofauti za utokeaji wa michakato ya kisemantiki kati ya maneno yenye asili ya Kiingereza na yale yenye asili ya Kiarabu. Utafiti huu uliongozwa na nadharia mbili ambazo ni Nadharia ya Alama na Nadharia ya Sarufi Amilifu. Kwa kiasi kikubwa data zilikusanywa kwa kutumia mbinu ya maktabani ambapo data zilizopatikana kwa mbinu hiyo ndio zilipelekwa uwandani kuhakikiwa kwa kutumia mbinu za hojaji na usaili. Uchambuzi wa data ulitumia mbinu ya uchambuzi mada ambapo maelezo ndio yametumika kwa kiasi kikubwa japo kulikuwa na matumizi ya kanuni, majedwali na vielelezo. Matokeo ya utafiti huu yanadhihirisha kuwa maneno ya mkopo yaliyomo katika Kiswahili yanaweza kubainishwa kwa kutumia njia za kileksikografia, kifonolojia na kimatamshi. Vilevile, utafiti huu umebaini kuwa tunaweza kuibainisha michakato mikuu minne ya kisemantiki kwa kutumia kanuni mbalimbali. Mathalani, kuna kanuni ya kubainishia Mchakato Panuzi wa Kisemantiki (MPK), Mchakato Finyazi wa Kisemantiki (MFK), Mchakato Geuzi wa Kisemantiki (MGK) na Mchakato Kapa wa Kisemantiki (MKK). MFK umeonekana kuchakata idadi kubwa ya maneno ya mkopo kuliko mingine. MFK umechakata 84% ya maneno yenye asili ya Kiingereza na 64% ya maneno yenye asili ya Kiarabu. Mchakato unaofuatia ni MPK umechakata 8% ya maneno yenye asili ya Kiingereza na 20% yenye asili ya Kiarabu. MGK umechakata 0% ya maneno yenye asili ya Kiingereza na 14% yenye asili ya Kiarabu ilhali MKK umechakata 8% ya maneno yenye asili ya Kiingereza na 2% yenye asili ya Kiarabu. Pia, matokeo yameonesha kuwa kuna sababu mahususi za kutokea kwa michakato ya kisemantiki kwenye maneno ya mkopo na utokeaji wa michakato hiyo katika maneno ya mkopo unatofautiana kati ya lugha kopwaji moja na nyingine. Aidha, utafiti huu unapendekeza kuwa tafiti fuatishi ziangalie michakato ya kisemantiki katika maneno yenye asili ya Kibantu katika Kiswahili, kwani utafiti huu umechunguza yale tu yenye asili ya Kingereza na Kiarabu.